Monday 6 March 2017

Ray Ashindwa Kuishi na Chuchu

 DAR ES SALAAM: Pamoja na kumzalia mtoto wa kiume aitwaye Jaden, staa wa sinema za Kibongo, Vincent Kigosi ‘Ray’ anadaiwa kushindwa kuishi na mwandani wake, Chuchu Hans ambaye naye ni mkali wa Bongo Muvi, kisa kikielezwa kuwa ni mama wa jamaa huyo ambaye hataki mwanaye aishi mbali naye.
 Habari za kuaminika zilieleza kuwa, Chuchu amekuwa akitangaza kwamba, amefunga ndoa na Ray lakini jamaa huyo amekuwa akikanusha hivyo mwanamama huyo kuwa kwenye wakati mgumu.
Hata hivyo, habari za ndani zilieleza kuwa, Ray ambaye amempangishia nyumba Chuchu maeneo ya SinzaDarajani, Dar amekuwa akienda nyumbani hapo kwa mzazi mwenzake lakini kila inapofika usiku wa manane huwa anamkimbia na kurudi kulala nyumbani kwa mama yake, Sinza-Mori, Dar. “Yaani hakuna kitu kinachomuumiza Chuchu kama hicho.
Lakini kibaya zaidi Ray amekuwa na msimamo mkali kwamba hawezi kumwacha mama yake na kwenda kuishi na Chuchu. Mbali na hilo pia Ray hawezi kuishi na Chuchu pale kwa mama yake kwa sababu kuna mambo hayajakaa vizuri kati ya Chuchu na mamamkwe wake,” kilisema chanzo chetu na kuongeza:
“Ray anapaswa kumaliza tatizo hilo ili mtoto wao apate malezi ya baba na mama kwa saa ishirini na nne.”
Wikienda lilipomtafuta Ray alikiri kushindwa kuishi au kukaa na Chuchu kwa muda wote kutokana na ukweli kwamba, mama yake hapendi ahame nyumbani na kwenda kupangisha kwani yeye ni kama ‘mume’ wa mama yake kwani ni mtoto wa mwisho hivyo anamuangalia mama yake.
“Ni kweli ninaishi nyumbani kwetu, siyo kama sina nyumba na kuishi nyumbani siyo dhambi. Uwezo wa kupanga ninao lakini mama yangu hapendi nihame nyumbani kwetu.
“Ni kweli mama mtoto wangu (Chuchu) anaishi kwake na mimi ninaishi nyumbani kwetu. Mama yangu alishaniambia hata nikihama atakuja kuishi na mimi nyumbani kwangu.
“Chuchu Hans anajua kuhusu hilo ndiyo maana hata nyumba anayoishi nimempangia mimi,” alisema Ray aliyelelewa na mama yake pekee tangu baba yake alipofariki dunia wakati staa huyo akiwa na umri wa miaka nane.
Wikiendi iliyopita Ray alizindua sinema yake mpya ya Gate Keeper ambayo alieleza kwamba imelenga kuvunja ukimya wake wa muda mrefu tangu alipofariki dunia, mshindani wake kwenye soko la sinema za Kibongo, Steven Kanumba mwaka 2012.

No comments:

Post a Comment